Gari ndogo yenye nambari za usajili Z
897 DF ikionekana kuvurugika kabisa baada ya kifusi cha dari ya jengo la
Makumbusho ya Taifa la Beit al ajaib kuidondokea kufuatia mvua za vuli
zinazoendelea kunyesha Zanzibar.
Sehemu ya jengo la Makumbusho ya Taifa
la Beit Al Ajaib ikionekana kunyofuka kutokana na mvua za vuli
zinazoendelea kunyesha Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Iddi akijaribu kuchungulia baadhi ya sehemu ya Jengo la
Makumbusho ya Taifa ambalo nyuma ya jengo hilo limepata maafa ya
kubomoka.Nyuma ya Balozi Seif ni Waziri wa Habari Utamaduni, Utalii na Michezo Mh. Said Ali Mbarouk.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Iddi akiangalia sehemu ya jingo la beit al ajaib ambayo
imebomoka kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha Zanzibar.
--
Wakati neema ya mvua za vuli ikiendelea kunawiri katika maeneo mbali mbali nchini ikileta faraja zaidi
kwa wakulima na wafugaji kwa kupata malisho ya Mifugo yao lakini kwa
upande mwengine mvua hiyo hiyo imeonekana kuleta hasara.
Hasara hiyo
inaonekana kuikumba Wizara ya Habari,Utamaduni, Utalii na Michezo
kufuatia Jengo lake Maarufu la Makumbusho ya Taifa la Beit Al- Ajaib
liliopo Forodhani Mjini Zanzibar kubomoka upande wa nyuma wa Jengo hilo.
Kifusi kilichodondoka kutoka kwenye Dari ya Jengo hilo robo yake kimeishia kwenye
gari moja ndogo yenye nambari za usajili Z 897 DF inayomilikiwa na
Bwana Said Saleh Saidi Mkaazi wa Forodhani ambae alikuwa ameiegesha
pembezoni mwa Jengo hilo.
Makamu wa Pili wa
Rais wa Zanzibar Balozi Seif alifika mapema Juzi asubuhi katika eneo hilo
kuangalia tukio hilo baada ya kupata taarifa hiyo na kuonyesha
masikitiko yake kutokana na hasara hiyo kubwa.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mh. Said Ali Mbarouk alimueleza Balozi Seif kwamba Wizara hiyo ilikuwa ikiendelea na juhudi za kulifanyia matengenezo Jengo hilo kwa kipindi kirefu sasa.
Waziri Mbarouk alifahamisha kwamba jitihada hizo zilikuwa zikienda sambamba na matayarisho ya kutaka kuliezeka jengo hilokwa upande wa nyuma.
Alieleza kwamba
kutokana na tatizo hilo Wizara ya Habari inakusudia kuwatumia Wataalamu
wa Wizara yake kwa kukaa pamoja na Wahandisi wa Idara ya Ujenzi Zanzibar
kuangalia hatua za kuchukuwa ili tatizo hilo lisije leta maafa.
Naye Mmiliki wa
gari ndogo iliyoegeshwa pembezoni mwa Jengo hilo ambayo imeharibika
kabisa kutokana na tukio hilo Bwana Said Saleh Said alisema alishuhudia
mporomoko huo ukitokea muda mfupi baada ya kuegesha gari yake.
Bwana Said
alimueleza Balozi Seif kwamba Tukio hilo liliweza kuleta mtafaruk na
kusababisha hofu miongoni mwa wakaazi wa eneo hilo pamoja na wale
wafanyakazi wa Jengo hilo.
Makamu wa Pili wa Rais wa ZanzibarBalozi Seif Ali Iddi akimpa
pole Bwana Said kutokana na hasara iliyomkumba alimtaka kuendelea kuwa
na subra na kuamini kwamba hiyo ni mitihani ambayo inaweza kutokea na
kumpata kuimbe ye yote na wakati wowote ule.
Hata hivyo Balozi
Seif aliwanasihi watu wanaomiliki vyombo vya moto kuhakikisha kwamba
wanakata bima ya vyombo vyao kwa lengo la kujinginga na hasara wakati
vyombo vyao vinapopatwa na ajali.
Jengo la Beit Al- Ajaib lililojengwa na
Utawala wa Kijerumani Mwaka 1870 likiwa na umri wa karibu miaka 142
hutegemewa sana katika Sekta ya Utalii ndani ya mwambao wa Afrika
Mashariki pamoja na wataalamu na wanafunzi wa kigeni wanaokuja kufanya
utafiti hapa Nchini.
Na
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
No comments:
Post a Comment
This is a public viewable website, post something that is not harmful to other people