POLISI sita na raia 138 wameuawa kwenye matukio ya ujambazi wa kutumia silaha, kati ya Januari na Septemba mwaka huu.
Kutokana
na hali hiyo, Serikali imetoa siku 30 kuanzia leo kwa watu wote
wanaomiliki silaha kinyume cha utaratibu kuzisalimisha kwa hiari yao,
ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.Hayo yalibainishwa jana na
Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi.
Dk Nchimbi alisema
hatua hiyo inatokana na kuongezeka kwa matukio ya uhalifu wa kutumia
silaha, kwani tangu Januari hadi Septemba mwaka huu kumebainika kuwapo
kwa matukio 876.
“Matukio hayo yamesababisha vifo vya raia 138 na
polisi sita, mali zenye thamani ya Sh4,560,389,970 ziliibwa kwa kutumia
silaha zinazomilikiwa kinyume cha sheria, zikiwamo nyingine
zinazomilikiwa kisheria lakini zinatumika isivyo halali,” alisema Dk
Nchimbi na kuongeza:
“Kufuatia hali hiyo natoa wito kwa mtu
yeyote au kikundi chochote kinachomiliki silaha kinyume cha sheria
kuisalimisha vituo vya polisi, kwa wenyeviti wa vitongoji/vijiji,
watendaji wa kata, taasisi za dini, wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa.”
Alisema atakayesalimisha silaha kwa hiyari ndani ya kipindi hicho hatachukuliwa hatua zozote za kisheria.
“Kwakweli
baada ya muda huo kumalizika yaani Januari 5, mwakani operesheni kali
itafanyika nchi nzima na yeyote atakayebainika akimiliki silaha isivyo
halali na kinyume cha sheria atakamatwa na sheria itachukua mkondo
wake,” alisema Waziri Nchimbi.
No comments:
Post a Comment
This is a public viewable website, post something that is not harmful to other people